TANI 18 ZA DHAHABU ZAPOTEA KILA MWAKA, NANI ALAUMIWE.

Dodoma.Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imefichua kuwapo kwa utoroshaji mkubwa wa madini unaofanywa na baadhi ya wachimbaji wadogo na kubainisha tani 18 za dhahabu hutoroshwa kila mwaka kwenda nje.
Akiwasilisha taarifa ya kamati hiyo Bungeni jana, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Victor Mwambalaswa alisema taarifa kutoka kwa Wakala wa Ukaguzi wa Madini Tanzania (TMAA) zinathibitisha utoroshaji huo wa madini.
“Kwa taarifa kamati ilizozipata kutoka TMAA ni kuwa kiasi cha madini kinachochimbwa nchini mwetu na kutorosha nje ya nchi ni kingi kuliko takwimu,” alisema mwenyekiti huyo.
“Kwa mfano takribani tani 20 za dhahabu huzalishwa kila mwaka na wachimbaji wadogo lakini takwimu rasmi za Serikali za uzalishaji ni chini ya tani mbili kwa mwaka,” alisema.
Kamati hiyo imeshauri kwa kuanzia, eneo lote la Migodi ya Mirerani liwekewe uzio ili eneo hilo liwekewe ulinzi kwa kutumia watu na mitambo maalumu ili kuhakikisha kila kipande kinachotoka kinahakikiwa na kulipa tozo na ushuru.
Wakati huohuo, Sakata kusafirishwa kwa gesi kutoka Mtwara kwenda jijini Dar es Salaam, limeibuka tena bungeni ambapo wabunge wawili wa Mkoa wa Lindi, wamesema kutotekelezwa kwa ahadi za muda mrefu ndiko kunakosababisha mgogoro.
Wameyasema hayo bungeni jana wakati wakichangia taarifa za Kamati za Bunge za Miundombinu pamoja na ile ya Nishati na Madini kuhusu utekelezaji wa shughuli zake kwa mwaka 2010.
Mbunge wa Mchinga, Said Mtanda (CCM), alisema wananchi wa mikoa ya Lindi na Mtwara hawana tatizo na kusafirishwa kwa gesi kwenda Dar es Salaam. Alisema wananchi wa mikoa hiyo wanahoji juu ya baadhi za ahadi za serikali ambazo zimetolewa kwa muda mrefu lakini hazijatekelezwa.
“Ahadi zilizoahidiwa hazijatekelezwa, lakini mradi huu kwa kipindi cha mwaka unaelekea kukamilika, lakini ahadi hizo hazijafanyiwa kazi, inashangaza bomba la gesi lifike Dar es Salaam lakini vijiji vya mikoa ya lindi havina umeme,’alisema.
Alisema jimbo lake lina umeme katika vijiji viwili, lakini waliahidiwa kupatiwa umeme tangu mwaka 2010 mpaka leo hakuna hata dalili ya nguzo zilizowekwa.
Aliitaka Serikali kutimiza ahadi zake kwa wananchi wa mikoa hiyo na kuangalia upya kuhusiana na viwango vya fidia kwa watu wanaohamishwa kwenye maeneo yao.
Mbunge wa Lindi Mjini, Salum Barwany (CUF), alisema kuwa mambo yote yanayofanywa na serikali yanafaa kujulikana kwa wabunge kwasababu ndio wawakilishi wa wananchi.

Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright WORLD OF TODAY Published.. Blogger Templates
Back To Top