WAKATI wa mahojiano yao na CNN, Patsy hakuwa mzungumzaji
lakini baadaye alisema kwa kifupi kwamba anaamini muuaji wa binti yao yupo na
hajakamatwa tu.
Polisi wa mji wa Boulder hawakufurahishwa na maelezo ya
familia ya Ramsey wakati akizungumza na CNN, siku iliyofuata Meya wa mji huo na
maofisa wa polisi waliitisha mkutano na vyombo vya habari ambapo walikanusha
kauli iliyotolewa na mke wa Ramsey aliposema kwamba muuaji wa binti yao yupo na
hajakamatwa. Maofisa hao walisisitiza kwamba mauaji ya JonBenet siyo endelevu,
hivyo waliwataka wakazi wa mji huo kulala kwa amani bila hofu kwa sababu
hakutatokea mauaji kama hayo tena.
Maofisa hao walidai kwamba wanamjua aliyemuuwa mtoto
JonBenet Ramsey na bado kitambo kidogo watathibitisha madai yao.
Kwa muda mfupi polisi walihamisha hisia zao kuwatuhumu John
na Patsy Ramsey na mauaji ya binti yao na kuelekeza hisia zao hizo kwa watoto
wake aliowazaa katika ndoa yake ya awali, wanaoitwa Melinda na John Andrew
Ramsey.
Pamoja na minong’ono iliyoenea kwamba walionekana katika mji
huo wa Bouliver siku ya Krismas, lakini wote walidai kwamba walikuwa Atlanta
siku hiyo ya Desemba 25 na siku iliyofuata yaani Desemba 26, waliondoka katika
mji huo kuelekea katika mji wa Minneapolis ambako walipanga kukutana na baba
yao pamoja na mama yao wa kambo na wanawe katika nyumba yao wanayoitumia wakati
wa likizo hapo Minneapolis, hata hivyo rafiki mmoja wa familia aliwapigia simu
na kuwajulisha kwamba mtoto JohnBenet ametekwa nyara na hajulikani alipo.
Walipanda ndege hadi katika mji wa Denver na hapo walikodi teksi hadi Boulder.
Polisi waliyachukua maelezo yao na kutokana na kutokuwa na
muunganiko na tukio hilo, walibadilisha hisia zao kutoka kwa watoto hao na
kuwageukia John na Patsy Ramsey wazazi wa mtoto JonBenet.
Lakini Februari 8, mwaka 1997 kitengo cha kuzuia uhalifu cha
Boulder kilitangaza kwamba familia ya Ramsey itatoa zawadi ya dola 100,000 za
Marekani kwa mtu yeyote atakayejitokeza kutoa taarifa zitakazosaidia kukamatwa
kwa muuaji na kuhukumiwa.
Rais wa kitengo cha kuzuia uhalifu cha kimataifa Larry Wieda
alifafanua juu ya hatua hiyo. “Tunachofanya ni kuhakikisha hakuna taarifa
zinazotupita juu ya tukio hili.” Aliendelea kusema kwamba kwa kawaida taasisi
anayoiongoza huwa inatoa zawadi inayofikia dola 10,000 za Marekani, lakini
akaongeza kwa kusema; “Siwezi kukumbuka kesi yoyote ambayo ilipatiwa ufumbuzi
kutokana na kiasi kikubwa cha zawadi kilichoahidiwa.”
Hata hivyo kiwango hicho kilichotangazwa na familia ya
Ramsey kiliamsha mwamko kutoka kwa jamii ya Wamarekani kutoa taarifa kwenye
taasisi hiyo ya kuzuia uhalifu. Kwa muda mfupi taasisi hiyo ilipokea simu zaidi
ya 1,500 kutoka kwa raia wema ambao walidai kwamba wana taarifa ambazo
zitasaidia kupatikana kwa muuaji. Mpaka
kufikia katikati ya Februari, polisi walikuwa wamepokea barua zipatazo 1,000 na
simu zapatazo 3,000. Polisi walisema kwamba kati ya hizo taarifa ni asilimia
tano tu ambazo zinaonekana huenda zikazaa matunda, lakini pia
waliwatahadharisha wananchi kutowapotezea muda polisi. Kauli hiyo ilitokana na
baadhi ya taarifa kuonekana zisizo na mashiko. Akitolea mfano baadhi ya taarifa
hizo ni pamoja na zile ambazo wapo waliodai kwamba wana uwezo wa kufanya
miujiza na kumbaini muuaji.
Kuanzia hapo, olisi hawakutoa taarifa zozote kwenye vyombo
vya habari kuhusiana na kesi hiyo, na upelelezi wa kesi hiyo ulionekana
kufanywa kwa siri. Wakati John Meyer wa kitengo cha uchunguzi wa maiti katika
wilaya ya Boulder alipomaliza uchunguzi wa mwili wa JonBenet Ramsey hapo
Februari 11, mwaka 1997, alikataa kutoa taarifa kwa undani kuhusiana na matokeo
ya uchunguzi wake akidai kwamba askari wa upelelezi wa mji huo wa Boulder
pamoja na waendesha mashitaka wanaohusika na kesi hiyo walimuonya kwamba, iwapo
atatoa matokeo ya uchunguzi wake ataathiri kwa kiasi kikubwa mwenendo wa
upelelezi wao katika kumtafuta muuaji.
Msemaji wa kitengo hicho cha uchunguzi wa maiti alisema
kwamba, miongoni mwa taarifa za uchunguzi wa mwili wa binti huyo ambazo polisi
na ofisi ya mwanasheria wa wilaya ambazo wasingependa ziwekwe hadharani ni
kuhusu majeraha mangapi yamekutwa kwenye mwili wa marehemu, idadi ya vielelezo
vilivyokusanywa baada ya uchunguzi, na mbinu iliyotumiwa na muuaji kutekeleza
mauaji hayo (details of the Modus operand of the killer)
Hata hivyo kuna taarifa iliyovuja kutokana na uchunguzi wa
mwili wa binti huyo ni kwamba, mwili wa binti huyo ulikutwa ukiwa na michubuko
ya muda mrefu katika uke ambapo ripoti hiyo ilieleza kwamba michubuko hiyo
inawezekana ilitokana na binti huyo kunajisiwa mara kwa mara.
Haraka sana msemaji wa familia ya Ramsey Pat Korten
alizungumzia tuhuma hizo na alimshirikisha aliyekuwa daktari wa binti huyo ambaye alikanusha, kwamba hajawahi
kuona ushahidi wowote kwa binti huyo unaoonyesha alikuwa akinyanyaswa kijinsia.
Mwezi huo wa Februari haukuwa mzuri sana kwa familia ya
Ramsey, kutokana na jinsi polisi walivyokuwa wakiizungumzia kesi ya binti yao
na kusababisha uhusiano wa familia ya Ramsey na polisi kutokuwa mazuri.
- See more at:
http://raiamwema.co.tz/mauaji-ya-ajabu-ya-mtoto-jonbenet-ramsey-iii#sthash.68KJCcDU.dpuf


Post a Comment